“Tubuni
basi mkarejee…dhambi zenu zifutwe zipate kuja nyakati za kuburudishwa” Matendo ya Mitume
3:19
Mtu mmoja aliwahi kusema “Haujawahi
kutokea ugonjwa hatari duniani kama dhambi.” Idadi ya watu waliopoteza maisha
kwa ajili ya dhambi ni kubwa kuliko idadi ya watu waliokufa kwa ajili ya
Malaria na UKIMWI.
Katika Warumi 6:23 inasema mshahara wa
Dhambi ni mauti. Neno mshahara hapa laweza kutafsiriwa kuwa “malipo ya ya
dhambi ni kifo.” Neno kifo pia laweza
kutafsiriwa kuwa mtu kukosa furaha, maendeleo, kukosa amani nk. Hivyo ni kusema
malipo ya Dhambi ni ugumu wa maisha, magonjwa kama vile (HIV/AIDS), kukosa
maendeleo, kukosa amani, ndoa kuvunjika, kuongezeka kwa ajali, mauaji, ugaidi
nk.
Tangu anguko la mwanadamu pale Edeni
maisha yamekuwa ya kukatisha tamaa, majuto nk. Katika dunia nzima kila mtu
anatamani kupata maisha mazuri ya amani, maendeleo, furaha, afya nk. Dawa ya
kusaidia kuondoa dhambi ambayo ndiyo asili ya mabaya yote inatafutwa. Mtume
Paulo anakutana na mazingira kama hayo na anatoa majibu kwa kusema “TUBUNI.”
Nini maana ya neno hilo? Neno “Tubu”
linamaanisha “Geuka” “badili mwelekeo” kama ulikuwa unaenda kushoto geuka uende
kulia. Kwa minajili hiyo neno hili linatuita kuyaacha yote yanayotufanya
tumkosee Mungu na kuyatenda yale yanayompendeza yeye.
Petro anatufundisha katika 1Petro
3:10-11 juu ya toba inayoleta matunda. Jiulize wewe unatafuta wapi maisha
mazuri? Anasema maisha mazuri na siku njema huja kwa:
i. Kuzuia ulimi usinene mabaya
ii. Midomo yako isinene uwongo
iii. Acha mabaya tenda mema
iv. Tafuta amani, uifuate sana
Leo kweli wengi tumegeukia kutafuta maisha na
siku njema kwenye rushwa, waganga, ufisadi, umalaya, ugaidi, wizi, uchawi,
utapeli nk. Neno la Mungu linasema tubu yaani geuka-usitende hayo tena.
Tunapotubu Mungu anamtuma Yesu kwa njia
ya Roho wake Mtakatifu kutuburudisha. Tena kwa njia hiyo tunapata baraka.
Historia ya maisha yetu inabadilika. Badala ya kilio huja kicheko, badala ya
laana huja baraka.
Ndugu mpendwa wako mamilioni ya watu
ambao wamegundua siri hii kwa kufanya hivyo wamebadili historia ya Maisha yao.
Sasa wanayo furaha na Tumaini la maisha ya hapa duniani na hata baadaye huko
mbinguni. Ni vyema ukaisikia sauti ya Mungu inayokuita wewe kutubu (geuka) sema
sala hii Bwana atakusikia na kukufanya kiumbe kipya.
“Mungu baba yetu wa
mbinguni, nasogea mbele zako nikiyajutia maovu yangu yote. Nakuomba unirehemu na
kunisafisha na uovu wangu wote unipe nguvu ya Roho wako mtakatafu ili
aniwezeshe kuwa na mwenendo mpya wa kukupendeza wewe. Tangu leo niwe mwana
wako. Kwa Kristo Bwana wetu”. Amen.
Sasa umekuwa kiumbe Kipya. Ikiwa
unahitaji msaada zaidi waweza kwenda kwa kiongozi wa kanisa lililoko karibu
nawe au kupiga simu kwa namba zifuatazo.
0754855769
0752010436
0763997146
0769165722
0765750523
0 comments:
Post a Comment